Pages

Subscribe:

Wednesday 21 January 2015

mwanzo Kolamu Kolamu Fidel Castro; mtoto wa ‘housegirl’ aliyekabili vigingi vingi kwenda Ikulu- 2


Wiki iliyopita tuliona Fidel Castro alikwama kwenye ndoto yake ya kugombea ubunge baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Generali Fulgencio Batista na kuvuruga demokrasia.
Castro hakukubaliana na mapinduzi hayo na alikuwa miongoni mwa walioupinga utawala wa Batista na mara kadhaaa alijaribu kutumia sheria pasipo mafanikio.
Leo tutaona jinsi Castro alivyoasi na kuunda kikosi chake cha wanamgambo dhidi ya Generali Batista. Alifanya shambulio lake la kwanza Julai 26, 1953 akiwa na askari 160 katika kambi kubwa ya jeshi ya Moncada jijini Santiago de Cuba.
Katika shambulio hilo, alilipoteza askari wapatao 60 huku yeye mwenyewe akikamatwa na kuhukumiwa kunyongwa.
Kabla ya utekelezaji wa hukumu alibadilishiwa hukumu na kufungwa miaka 15 jela. Baadaye aliachiwa  na kutorokea Mexico na kujenga kikosi imara cha uasi ambacho kilirudi na kuushambulia utawala wa Generali Batista Desemba 2, 1956.
Askari wake wengi waliuawa kutokana na upinzani mkubwa wa majeshi ya Serikali kiasi cha yeye mwenyewe pamoja na ndugu yake Raul pamoja na swahiba wake mkubwa, Che Guevara kukimbia.
Kwa miaka miwili alijipanga na kuendesha vita ya msituni ambayo ilimwongezea watu waliomuunga mkono kabla hajamshinda hasimu wake aliyekuwa anapoteza mvuto wa kisiasa.
Mwaka 1959 Generali Batista alishindwa vita na kukimbia. Baada ya miezi sita Castro alichaguliwa kuwa Rais ikiwa ni baada ya miezi sita ya kushikilia wizara ya ulinzi.
Aprili 1959, alizuru Marekani lakini Rais wa wakati huo, Dwight Eisenhower aligoma kumpokea wala kukutana naye. Suala hilo liliongeza uhasama baina ya nchi hizo mbili. Marekani ilivunja uhusiano wa kidiplomasia na Cuba Januari, 1961.
Uamuzi huo haukumtisha Castro kwani miezi mitatu baadaye aliutangazia ulimwengu kuwa nchi yake ni ya kijamaa na kuanzia hapo akaelekeza nguvu kwa dola ya Urusi aliyotiliana nayo saini mikataba mingi ya biashara na maendeleo.
Aprili 1961, utawala wa Castro ulivamiwa katika eneo maarufu la ‘Bay of Pigs’ lakini alifanikiwa kuwadhibiti waasi hao kwa kuwakamata mamia ya askari huku akiua maelfu. Marekani ilikanusha kuhusika.
Aliwekewa vikwazo vya kiuchumi ikiwamo biashara ya kuiuzia Marekani sukari lakini hakulegeza msimamo. Pamoja na kuanguka kwa dola ya Urusi, bado Cuba ni nchi ya kijamaa licha ya Castro kung’atuka kwa hiari yake kutokana na kudhoofu kwa afya yake, Februari 19, 2008.
Alimwachia madaraka kaka yake Raul Castro. Raul yeye alipunguza misimamo yake na hata kuamua kurejesha uhusiano na Marekani.


Chanzo: Mwanananchi

0 comments:

Post a Comment