Wiki iliyopita tuliona Fidel Castro alikwama
kwenye ndoto yake ya kugombea ubunge baada ya mapinduzi ya kijeshi
yaliyoongozwa na Generali Fulgencio Batista na kuvuruga demokrasia.
Leo tutaona jinsi Castro
alivyoasi na kuunda kikosi chake cha wanamgambo dhidi ya Generali
Batista. Alifanya shambulio lake la kwanza Julai 26, 1953 akiwa na
askari 160 katika kambi kubwa ya jeshi ya Moncada jijini Santiago de
Cuba.
Katika shambulio hilo, alilipoteza askari wapatao 60 huku yeye mwenyewe akikamatwa na kuhukumiwa kunyongwa.
Kabla ya utekelezaji wa hukumu
alibadilishiwa hukumu na kufungwa miaka 15 jela. Baadaye aliachiwa na
kutorokea Mexico na kujenga kikosi imara cha uasi ambacho kilirudi na
kuushambulia utawala wa Generali Batista Desemba 2, 1956.
Askari wake wengi waliuawa
kutokana na upinzani mkubwa wa majeshi ya Serikali kiasi cha yeye
mwenyewe pamoja na ndugu yake Raul pamoja na swahiba wake mkubwa, Che
Guevara kukimbia.
Kwa miaka miwili alijipanga na
kuendesha vita ya msituni ambayo ilimwongezea watu waliomuunga mkono
kabla hajamshinda hasimu wake aliyekuwa anapoteza mvuto wa kisiasa.
Mwaka 1959 Generali Batista
alishindwa vita na kukimbia. Baada ya miezi sita Castro alichaguliwa
kuwa Rais ikiwa ni baada ya miezi sita ya kushikilia wizara ya ulinzi.
Aprili 1959, alizuru Marekani
lakini Rais wa wakati huo, Dwight Eisenhower aligoma kumpokea wala
kukutana naye. Suala hilo liliongeza uhasama baina ya nchi hizo mbili.
Marekani ilivunja uhusiano wa kidiplomasia na Cuba Januari, 1961.
Uamuzi huo haukumtisha Castro
kwani miezi mitatu baadaye aliutangazia ulimwengu kuwa nchi yake ni ya
kijamaa na kuanzia hapo akaelekeza nguvu kwa dola ya Urusi aliyotiliana
nayo saini mikataba mingi ya biashara na maendeleo.
Aprili 1961, utawala wa Castro
ulivamiwa katika eneo maarufu la ‘Bay of Pigs’ lakini alifanikiwa
kuwadhibiti waasi hao kwa kuwakamata mamia ya askari huku akiua maelfu.
Marekani ilikanusha kuhusika.
Aliwekewa vikwazo vya kiuchumi
ikiwamo biashara ya kuiuzia Marekani sukari lakini hakulegeza msimamo.
Pamoja na kuanguka kwa dola ya Urusi, bado Cuba ni nchi ya kijamaa licha
ya Castro kung’atuka kwa hiari yake kutokana na kudhoofu kwa afya yake,
Februari 19, 2008.
Alimwachia madaraka kaka yake Raul Castro. Raul yeye alipunguza misimamo yake na hata kuamua kurejesha uhusiano na Marekani.
Chanzo: Mwanananchi
0 comments:
Post a Comment