Ballali alilazwa katika hospitali mbili tofauti kabla ya kufariki dunia.
Neville Meena, Mwananchi
Taarifa za Idara za Serikali ya Marekani
zinathibitisha kwamba aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT),
Daudi Ballali alifariki dunia akiwa Washington DC, akiwa na umri wa
miaka 66.
Gazeti hili lilianza kufanya uchunguzi kuhusu
ukweli wa kifo cha Ballali miaka miwili iliyopita, kutoka na kuwapo kwa
mkanganyiko na sintofahamu kuhusu kifo hicho, vilivyosababishwa na jinsi
alivyoondoka nchini Agosti 2007, kuugua kwake, mazingira ya kifo na
hata usiri uliotawala mazishi yake.
Mbali na Mwandishi wa Mwananchi kufika alikozikwa kwenye Makaburi ya Gate of Heaven, eneo la Silver Spring, Maryland nchini Marekani mwanzoni mwa mwezi huu, taarifa rasmi za Serikali ya Marekani zinaonyesha kuwa Ballali alifariki dunia Mei 16, 2008.
Taarifa rasmi za idara zenye dhamana ya kutunza
rekodi mbalimbali za watu wanaoishi Marekani zinaonyesha kwamba mara ya
mwisho Ballali alikuwa akiishi Washington DC na alifariki akiwa na umri
wa miaka 66.
Taarifa hizo zinapatika katika Idara za Serikali
ya Marekani zinazotambuliwa kama United States Vital Records na United
States Public Records Index, ambazo zinahusisha majina ya watu, ndoa,
ndoa zilizovunjika, anwani za makazi yao ya sasa na walikowahi kuishi
kabla, namba ya huduma (social security number) na taarifa nyingine
muhimu.
Taarifa hizo zinaonyesha kuwa kabla ya kuishi
Washington DC, Ballali aliwahi kuishi Potomac, Maryland katika anuani
inayosomeka 11514 Seven Locks Rd, pia aliwahi kuishi Potomac, Maryland
20854 kwenye anuani 1801 45th St NW # 302 na pia Washington, Dc 20007
kwenye anuani za 13017 Parkland Dr na Rockville, Maryland 20853.
Rekodi hiyo namba 143502395 inawataja watu
wanaoweza kuwa na ukaribu na Ballali kuwa ni A. R. Ballali, Elizabeth T.
Ballali, Octavio T. Ballali, Rachel J. Ballali. Pia zipo taarifa
zinazomtaja Anna Muganda kuwa mmoja wa watu wa karibu wa Ballali.
Ufuatiliaji uliofanywa Mwandishi wa Mwananchi
zimethibitisha kwamba Elizabeth ni dada yake na Ballali wakati Octavio
na Rachel ni watoto wa Gavana huyo aliowazaa na mke wa kwanza, Malva
Ballali ambaye ni Raia wa Agentina.
Inaaminika kuwa Anna, Malva, Octivio na Rachel
ndiyo wanaofahamu ukweli kuhusu kilichosababisha kifo cha Ballali,
lakini kwa nyakati tofauti watu hao wa karibu na marehemu hawakuwa
tayari kueleza kilichotokea.
Ndugu wa karibu wa Anna wanasema mwanamama huo
ambaye alikuwa na Ballali mpaka pumzi yake ya mwisho, hayuko tayari
kuzungumzia suala hilo na kwamba hapendi kabisa kukumbushwa uchungu wa
kifo cha mumewe.
Alisema baada ya kupata uthibitisho huo alimpigia Sokoine na kumjulisha kwamba taarifa hizo hazikuwa za kweli kwani mgonjwa alikuwa akiendelea vizuri baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa na kuruhusiwa kutoka hospitalini.
Juzi Mwandishi wa Mwananchi alijaribu kuwasiliana na Octavio na
mama yake, Malva, lakini wote kwa pamoja walirejesha ujumbe kwamba
hawana cha kuzungumza, kwani wao mbali na kwamba hawakuwahi kuishi
Tanzania, wasingependa kurejea machungu yaliyowakuta.
Simu kwa familia
Wakati hayo yakidhihiri, baadhi ya wanafamilia
Ballali wamesema walipigiwa simu mara kadhaa, wakiulizwa iwapo ndugu yao
huyo bado yuko hai au amefariki dunia.
Wakizungumza na Mwanadishi wa Mwananchi nchini
Marekani, baadhi ya ndugu wa Ballali walisema takriban miezi mitano
kabla ya kukutwa na mauti, walipokea simu hizo kutoka Ubalozi wa
Tanzania, Washington DC, ukihoji iwapo Gavana huyo alikuwa hai au
amekufa.
Walisema taarifa hizo ziliwashtua na hawakufahamu
sababu za kuulizwa huko kwani hata kama Ballali angekuwa amefariki
dunia, wao ndiyo walipaswa kutoa taarifa za kifo chake na siyo taarifa
hizo kutoka Tanzania.
“Mara ya kwanza tulipigiwa simu alfajiri kutoka
kwa Ofisa wa Ubalozi, Joseph Sokoine akituuliza kwamba amepata taarifa
kutoka nyumbani Tanzania kwamba Ballali amefariki dunia,” alisema mmoja
wa ndugu hao, jina tunalihifadhi kwa sasa na kuongeza:
“Baada ya kupata simu hiyo, nilimtafuta mke wa
marehemu (Mama Anna Muganda) wakati huo walikuwa bado wako Boston,
lakini ndiyo walikuwa wameruhusiwa kutoka Hospitali ya Massachusetts,
nilimuuliza kuhusu hali ya mgonjwa akasema hali yake ilikuwa ikiendelea
vizuri”.
Alisema baada ya kupata uthibitisho huo alimpigia Sokoine na kumjulisha kwamba taarifa hizo hazikuwa za kweli kwani mgonjwa alikuwa akiendelea vizuri baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa na kuruhusiwa kutoka hospitalini.
Ndugu huyo wa Ballali alisema baada ya wiki mbili,
walipokea tena simu kutoka kwa Sokoine na zamu hii waliwaambia kwamba
alikuwa amepokea simu kutoka Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa
Mataifa, New York, wakiuliza kuwapo kwa taarifa kuwa Ballali alikuwa
amefariki dunia.
“Baada ya kupokea simu hiyo tulifuatilia tena
Boston na tuliambiwa Ballali alikuwa mzima. Nilimuuliza Joseph
(Sokoine), kama mgonjwa angekuwa amefariki wakati huo, taarifa zilipaswa
kutoka upande gani? Maana kama mgonjwa tulikuwa naye sisi basi ndiyo
tulipaswa kuwapa taarifa zote na siyo nyumbani Tanzania kutuarifu sisi,”
alisema ndugu huyo.
Balozi Sokoine
Akizungumza na Mwandishi wa Mwananchi jana, Balozi
Sokoine ambaye hivi sasa Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, alikiri akiwa
ubalozini mara kadhaa waliipigia simu familia ya Ballali kwa lengo la
kufahamu maendeleo ya ugonjwa wake.
Balozi Sokoine alisema miongoni mwa watu ambao aliwahi kuzungumza nao wakati huo ni kaka wa Anna, Emmanuel Muganda ambaye alisema aliwapa ushirikiano wa kila aina kuwawezesha kupata taarifa wakati Ballali alipokuwa mgojwa.
“Nakumbuka kuwapigia simu ndugu wa marehemu Ballali na siyo mara
moja, lakini tulikuwa tunafuatilia maendeleo ya mgonjwa na tulikuwa
tunampigia simu mke wake, Mama Muganda na ndugu wengine walioko
Marekani,” alisema Balozi Sokoine.
Kuhusu iwapo waliwahi kuulizia taarifa za kifo cha
Ballali, balozi huyo alisema: “Nakumbuka pia tuliwahi kuulizia suala
hilo kutokana na rumors (uvumi) uliokuwa umeenea Tanzania kwamba Ballali
amefariki, kwa hiyo tulipowaulizia wanafamilia walituambia kwamba
alikuwa hai bado”.
Balozi Sokoine alisema miongoni mwa watu ambao aliwahi kuzungumza nao wakati huo ni kaka wa Anna, Emmanuel Muganda ambaye alisema aliwapa ushirikiano wa kila aina kuwawezesha kupata taarifa wakati Ballali alipokuwa mgojwa.
“Bwana Muganda (Emmanuel) nakumbuka wakati
tukifuatilia taarifa hizo alitusaidia sana kufahamu hali ya mgonjwa na
hata tulipomuuliza kuhusu rumors (uvumi) huo naye alisema walikuwa
wakiulizwa na ndugu wa Tanzania kuhusu suala hilo,” alisisitiza Balozi
Sokoine.
Kwa upande wake Muganda ambaye alipata kuwa Mkuu
wa Idhaa ya Kiswahili y Sauti ya Amerika (VOA), alikiri kupokea simu
kadhaa kutoka Ubalozi wa Marekani, lakini akasema hakuwa akikumbuka hasa
ni kitu gani alichoulizwa kuhusu ugonjwa wa Ballali.
“Yes (ndiyo) walikuwa wakipiga simu mara nyingi na
lilipojitokeza suala la uvumi wa kifo cha Ballali na wao kutuuliza,
tulihoji kwamba kwanini pengine taarifa hizi zisitoke kwenye familia
kwenda serikalini na badala yake wao ndio walikuwa wanauliza,” alisema
Muganda ambaye bado anaishi Marekani mpaka sasa.
Kuugua kwake
Baadhi ya ndugu na familia wa Ballali wanasema
wakati alipoondoka kwenda Marekani, Gavana huyo alikiwa mzima na kwamba
alilazwa baada ya vipimo alivyofanyiwa katika Hospitali ya
Massachusetts, Boston alikokwenda kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi.
Mjini Washington DC, gazeti hili liliambiwa kuwa
Ballali alikuwa amepanga kurejea Tanzania baada ya uchunguzi huo, lakini
baada ya kufanyiwa vipimo hivyo daktari wake alimlaza kutokana na
kubaini tatizo kwenye utumbo wake mpana.
Mmoja wa ndugu zake alidokeza kuwa tatizo
aliloliona daktari kupitia vipimo vya kitaalamu, lilikuwa ni tofauti
kabisa na tatizo halisi, hivyo alishauriana na mwenzake aliyekuwa
Washington hivyo kumtibu matatizo yote mawili.
Alifanyiwa upasuaji mkubwa na baada ya kupata
nafuu aliruhusiwa kurejea nyumbani na baadaye kurudi Washington DC,
lakini Aprili 2008 aliumwa tena na kulazwa katika Hospitali ya Chuo
Kikuu cha Georgetown. Alikaa hospitalini hapo hadi mwanzoni mwa Mei
mwaka huo, alipoambiwa na madaktari kwamba asingeweza kupona na kwamba
mauti ingemkuta katika wiki mbili.
Ballali alirejeshwa nyumbani kwake, Washington DC
ambako aliendelea kuugua na hatimaye kukutwa na mauti Mei 16, 2008,
kisha kuzikwa katika makaburi ya Gate of Heaven yaliyopo Silver Spring,
Maryland, Mei 23. Nyuma ya kifo chake aliacha maelekezo kwamba pindi
atakapofariki dunia, mwili wake usiwekwe hadharani kwa maana ya
kutizamwa na watu nje ya familia wala kusafirishwa kuja Tanzania kwa
ajili ya maziko.
Gazeti hili liliwasiliana na hospitali zote mbili ambako Ballali
aliwahi kulazwa, lakini lilijibiwa kwamba taarifa za mgonjwa huyo
zinaweza kutolewa tu ikiwa familia ndiyo inayozihitaji.
Mwisho.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment